Na Gideon Mwakanosya,Iringa.
KUTOPEWA kipaumbele kwa ofisi za
maafisa jamii na maendeleo katika bajeti kumetajwa kuwa miongoni mwa
mambo yanayochangia kwa kiasi kikubwa vitendo vya ukatili wa kijinsia
kuendelea kushamiri katika jamii.
Hayo yalibainishwa na
wanahabari walioko kwenye mafunzo ya masuala ya ukatili wa kijinsia
yanayofanyika mkoani Iringa yakiwa yameandaliwa na Chama cha waandishi
wa habari wanawake(Tamwa) ambapo washiriki wanatoka katika mikoa ya
Mbeya,Iringa,Njombe na Ruvuma.
Wanahabari hao walisema ofisi za
maafisa ustawi wa jamii zinakabiliwa na changamoto ya uhaba wa fedha
kutokana na halmashauri nyingi kutozipa kipaumbele ofisi hizo wakati wa
upangaji wa bajeti.
Mmoja wa wanahabari hao Geofray Nilahi
alisema wengi wa maofisa kutoka ofisi hizo wamekuwa wakilalamika kukosa
fedha na ndiyo sababu hawatekelezi majukumu yao ipasavyo na badala yake
wamebakia maofisini ambako kimsingi hawana kazi zaidi ya kupiga soga.
Nilahi
alisema uhaba huo wa fedha umesababisha maafisa hao kushindwa
kutekeleza majukumu waliyopewa ikiwemo utoaji elimu kwa jamii juu ya
madhara ya ukatili wa kijinsia hivyo kusababisha vitendo vya ukatili
kuendelea kukithiri.
“Tunaendelea kulalamikia ukatili wa
kijinsia na ukatili wa dhidi ya watoto kila kukicha,Wapo watu wenye
dhamana ya kushirikiana na jamii ambao kimsingi wangesaidia kupunguza
vitendo hivi lakini hawajapewa kipaumbelea katika bajeti.Hawawezi
kuifikia jamii kwakuwa ofisi zao hazina pefa”
“Ni vema watawala
na wale wanaopitisha bajeti wakaliona hili na kutambua athari
zake.Maafisa ustawi wa jamii na wale wa maendeleo ya jamii wanaweza kwa
kiasi kikubwa kuwezesha jamii kuishi maisha ya kuheshimiana na kupendana
iwapo watafanya kazi yao.Lakini ofisi zao zimesahaulika
kabisa.Imewalazimu kubaki ofisini na kukaa kwenye viti vya kuzunguka”
alisema Nihahi.
Naye Joachim Nyambo alisema ni wakati kwa wadau
wa masuala ya kijamii kujiuliza kwa kila mmoja ni kwa namna gani ameweza
kujitoa katika kuhakikisha anakomesha vitendo vya ukatili wa kijinsia
kwenye jamii inayomzunguka na iwapo hajafanya basi atambue kuwa ana deni
la kutekeleza hayo.
Kwa upande wake Tumaini Msowoya,alisema
bado katika jamii kuna matukio mengi ya ukatili wa kijinsia na pia
ukatili dhidi ya watoto ambao baadhi ya wanajamii wanaufanya pasipo
kujua kuwa wanakosea.
Msowoya aliutaja ukatili ambao bado
unaendelezwa kuwa ni pamoja na wanawake kupigwa na waume zao,wanawake
kutumikishwa sambamba na utakasaji kwa wanawake wanaofiwa na waume zao.
Mwisho.
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni (Atom)
Chapisha Maoni