0

  
MGOMBEA ubunge CCM jimbo la Songea mjini ,Leonidas Gama
 
 NA STEPHANO MANGO,SONGEA

 MGOMBEA ubunge kupitia chama cha mapinduzi CCM jimbo la Songea mjini ,Leonidas Gama amesema kuwa endapo wananchi watampa ridhaa ya kuwa mwakilishi wao kwenye Bunge la Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania atahakikisha kuwa Manispaa ya Songea inakuwa na umeme wa uhakika pamoja na viwanda ili kuinua uchumi kwa wakazi wa manispaa hiyo.
 
 Gama aliyasema hayo jana kwenye uzinduzi wa mikutano ya kampeni za Udiwani Ubunge na Urais kwa jimbo la Songea mjini uliyofanyika kwenye viwanja vya malori vilivyopo kata ya Majengo uliyohudhuliwa na mamia ya wakazi wa jimbo hilo.
 
Alisema kuwa Manispaa ya Songea ina maeneo mazuri ya kuweka viwanda hivyo atahakikisha kuwa anawatafuta wawekezaji ndani na nje ya nchi ambao watafika kujenga viwanda ambavyo vitaweza kutoa ajira kwa vijana.
 
Alifafanua zaidi kuwa pia atahakikisha kuwa kiwanda cha Tumbaku  ambacho kilishakufa siku nyingi kinafufuliwa na kuanza shughuli ya kukausha Tumbaku ya wakulima jambo ambalo limekuwa ni kero ya muda mrefu kwa wakulima wa zao hilo.
 
“Ndugu wananchi hakuna ubishi kuwa Manispaa ya Songea bado ipo nyuma kimaendeleo hivyo inahitaji mbunge mwadilifu na mchapakazi kama mimi ninayeyajua matatizo ya wakazi wa Manispaa ya Songea kwa mimi mzaliwa wa hapa na ni mtoto wenu mwenye uchungu wa kutaka kuwasaidia wanasongea “alisema Gama.
 
Alieleza kuwa mkoa wa Ruvuma ikiwemo Manispaa ya Songea ni maarufu kwa kilimo hivyo endapo atakuwa Mbunge atajitahidi kushauriana na watalaam mbalimbali kuhakikisha manispaa hiyo inakuwa na mipango yakinifu kwa kuwa na mazao mengine mbadala badala ya kutegemea zao la mahindi peke yake ikiwemo na kutafuta masoko.
 
Aidha Gama alieleza kuwa pia atashughulikia kwa karibu kero za wazee kwa kuhakikisha wanapata matibabu bila kuwepo usumbufu kwenye zahanati,vituo vya afya na Hospital pamoja na kujenga hoja bungeni kuwa wazee wote ni lazima wapate pesheni itakayoweza kuwasaidia kupunguza makali ya maisha yao.
   MWISHO.

Chapisha Maoni

 
Top