0



Na Stephano Mango,Songea

MGOMBEA wa nafasi ya Ubunge jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma kupitia tiketi ya chama cha Demokrasia na maendeleo(CHADEMA)Joseph Fuime,amesema kuwa endapo wananchi watampa ridhaa ya kuwa mwakilishi wao atahakikisha anafufua zao la tumbaku ambalo lilikuwa mkombozi mkubwa kiuchumi kwa wananchi wa wilaya ya Songea na Namtumbo.

Fuime aliyasema hayo wakati alipokuwa akiwahutubia wananchi waliofika kumsikiliza kwenye mkutano wa kampeni wa chama hicho uliofanyika katika viwanja  vya stendi ya malori iliyopo kata ya Majengo mjini Songea.

Alisema kuwa ufufuaji wa zao hilo utakwenda sambamba na ufufuaji wa kiwanda cha kusindika tumbaku cha SAMCU ambacho kilikuwa kinatoa ajira zaidi ya 3000 kwa wananchi na wakazi wa mkoa wa Ruvuma wakiwemo walemavu,vijana na wanawake.

Alisema kati ya mambo mengine atakayopambana nayo pindi atakapochaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Songea mjini atahakikisha anapigania suala la upatikanaji wa  umeme wa uhakika ili wawekezaji wengi waweze kujitokeza kuwekeza viwanda vidogo vidogo ambavyo vitasaidia kupunguza tatizo la ajira kwa vijana.

Aidha aliongeza kusema kuwa  atahakikisha anaboresha huduma za afya kwa kujenga Hospitali kubwa ya rufaa pamoja na kukomesha tatizo la wagonjwa kulala kitanda kimoja watu watatu watatu ambalo limekuwa kero kubwa kwa wagonjwa.

Naye mgombea wa nafasi ya Udiwani  wa kata ya Majengo iliyopo katika Manispaa ya Songea kupitia tiketi ya chama hicho,Idd Abdalah akizungumza katika mkutano huo amewaomba wananchi wamchague tena ili aweze kumalizia kazi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango chalami amayo itafadhiliwa na mfuko wa benki ya dunia.

Abdalah aliyataja mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha uongozi wake kuwa ni uingizwaji wa umeme kwenye shule ya msingi Songea,ujenzi wa jiko katika shule ya sekondari Mbulani,  ujenzi wa soko la majengo bila ya kumchangisha mwananchi yeyote pamoja na kushawishi taasisi za kifedha ikiwemo benki ya posta,Finca na benki ya wanawake kwa akili ya kusaidia kutoa mikopo kwa wananchi wa kata ya Majengo.

MWISHO




Chapisha Maoni

 
Top