0

 Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Lishe Tanzania(Panita) Tumaini Mikindo akifungua moja ya mikutano yake

NA STEPHANO MANGO,MBEYA
WADAU wa lishe nchini wametakiwa kushirikiana na kamati za lishe za Halmashauri zilizopo kwenye kila Wilaya ili kufanya kazi kwa pamoja na kuhakikisha kuwa hali ya watoto kupata utapiamlo au udumavu wa watoto unakwisha

Wito huo umetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Lishe Tanzania(Panita) Tumaini Mikindo alipokuwa akifungua warsha ya siku mbili ya kuwajengea uwezo wadau wa Lishe kutoka kwenye mikoa ya Iringa,Njombe,Ruvuma,Mbeya,Rukwa na Katavi inayofanyika kwenye ukumbi wa Gr City Hotel jijini Mbeya

Mikindo alisema kuwa jukumu la kujenga afya njema kwa watoto ni la kila jamii hivyo kila mmoja kwa nafasi yake atende haki kwa kutoa mchango wake wa kiafya na kuijenga jamii bora isiyo kuwa na matatizo ya kiafya

Alisema kuwa ni aibu kuona jamii zinawekeza nguvu kubwa ya kiuchumi na kilasilimali kwenye kutibu walioathirika na udumavu au utapiamlo badala ya kujikita kuhamasisha kuzuia magonjwa hayo ambayo hasa yanawakuta watoto wadogo na wale waliopo shule za msingi

Alifafanua kuwa jamii inaweza kuzuia magonjwa hayo kwa kuzingatia kanuni za lishe, kulima bustani ndogo ndogo za mboga, matunda, kuhifadhi vizuri chakula, kuhakikisha kuwa mama mjamzito kabla ya kujifungua anakula vizuri na akijifungua ananyonyesha mtoto wake kwa uhakika

Alisema kuwa kaya zenye matatizo ya lishe zinapaswa zitambuliwe na jamii ili ziweze kusaidiwa na kamati za lishe za wilaya kwani ndani ya kamati hizo kuna wajumbe ambao wanahusika na masuala ya lishe

Awali Mratibu wa Miradi wa Panita Jane Msagati akiwakaribisha washiriki alisema kuwa wadau wa lishe wanatakiwa kutambua kuwa wao ndio chachu ya kupatikana kwa takwimu za matatizo ya lishe kwenye maeneo yao kwani wao ndio wanaishi huko

Msagati alisema kuwa ili jamii iondokane na tabia ya kulalamika ukosefu wa lishe ni lazima wadau wa lishe watimize wajibu wao kwa kuwaelimisha namna ya upatikanaji wa mazao bora na utengenezaji wa  lishe bora kwenye maeneo yao

Kwa upande wake Mshiriki kutoka Wilaya ya Rudewa Samwel Mtitu alisema kuwa Serikali ilikuwa na nia njema ya kuanzisha Kamati za Lishe za Wilaya lakini zinashindwa kufanya kazi kwa kigezo cha kutokuwa na fedha za kuziendesha

Mtitu alisema kuwa ni muhimu Serikali ikatimiza wajibu wake ambao kimsingi ulijiwekea kwa lengo zuri la kuhakikisha kuwa utapiamlo na udumavu wa akili unakomeshwa kwa kushirikiana na wadau wa lishe waliopo kwenye maeneo yao
MWISHO
 

Chapisha Maoni

 
Top