0

KAMANDA WA POLISI MKOA WA RUVUMA MIHAYO MSIKHELA

NA STEPHANO MANGO,SONGEA

JESHI la Polisi Mkoani Ruvuma limemtia mbaroni Janati Haji (32) mkazi wa kijiji cha Rwinga Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma kwa tuhuma za kukutwa na meno sita ya tembo ambayo alikuwa ameyapakia kwenye pikipiki akitokea kijijini Rwinga kwenda Songea Mjini.  

Akizungumza na Tanzania Daima jana ofisini kwake Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma Mihayo Msikhela alisema kuwa tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki huko katika kijiji cha Rwinga.

Msikhela alisema kuwa inadaiwa siku hiyo ya tukio Askari Polisi  wa wilaya ya Namtumbo wakiwa katika msako maalumu walifanikiwa kumkamata Haji akiwa na Meno sita ya Tembo aliyokuwa amebeba kwenye pikipiki yenye namba ya usajili T448 CZT aina ya SAN LG.

Alifafanua zaidi kuwa inadaiwa haji alikuwa akiyasafirisha meno hayo ya Tembo kwenda Songea ambako inadaiwa ndiko alikokuwa anatarajia kuyauza.

Alisema kuwa Polisi kwa kushirikiana na maafisa wa Idara ya Wanyama pori wanafanya jitihada ili kupata thamani ya nyara hizo na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara tu upelelezi utakapo kamilika.

Kamanda Msikhela alisema kuwa Jeshi la Polisi mkoani humo bado linaendelea na msako mkali ili kuwabaini watu wanaojihusisha na biashara hiyo ya meno ya Tembo kwenye mbuga ya wanyama ya selou.

MWISHO

Chapisha Maoni

 
Top