KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, kikundi cha zaidi ya watu 40 wanaodaiwa kupandikizwa na Mbunge wa Jimbo la Mbinga, Gaudence Kayombo katika kijiji cha Ruanda kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kimewashambulia kwa kuwarushia mawe waandishi wa habari ambao wamenusurika kujeruhiwa vibaya, wakati walipokwenda kijijini hapo kutekeleza majukumu yao ya kikazi.
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo,
Mihayo Msikhela amezungumza na vyombo mbalimbali vya habari na kueleza kuwa
tukio hilo lilitokea Agosti 17 mwaka huu majira ya saa 6:30 mchana kijijini humo, ambapo waandishi hao walivamiwa
na kikundi hicho akiwemo na Mwenyekiti wa kijiji, Deograsias Haulle kwa kupigwa
na kurushiwa mawe.
Alisema Mwenyekiti Haulle ameumizwa
mdomoni na puani ambako alipigwa na jiwe na mtu asiyejulikana na kwamba
amepatiwa matibabu, katika hospitali ya wilaya hiyo na kuruhusiwa kurudi
nyumbani.
Msikhela aliwataja waandishi wa
habari mkoani Ruvuma, ambao walikumbwa na mkasa huo kuwa ni; Kassian Nyandindi
anayeandikia magazeti ya kampuni ya Businesstimes, Aden Mbelle na Pastory
Mfaume kutoka redio ya Jogoo FM iliyopo mkoani hapa mjini songea.
Alisema kuwa hali hiyo ilijitokeza
wakati wanahabari hao walipokwenda kutekeleza majukumu yao ya kikazi, kuandika
habari za tukio la kufungwa kufuli Ofisi za kata ya Ruanda na baadhi ya
wananchi ambao majina yao bado hayajapatikana.
Wakati walipokuwa wamekamilisha kazi
yao wakijiandaa kurudi, ndipo kundi hilo ambalo lilijitokeza ghafla
liliwashambulia waandishi hao na kwamba mwandishi wa habari Mbele, alipigwa
jiwe katika eneo la usoni upande wa kulia.
Kamanda huyo wa Polisi aliongeza
kuwa hivi sasa wamefanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja ambaye ni Daniel Komba
maarufu kwa jina la Gadaffi, ambaye anadaiwa kuongoza kikundi hicho na kuleta
vurugu hizo huku wengine wakiendelea kutafutwa, ili wachukuliwe hatua za
kisheria.
Vilevile Mkuu wa wilaya ya Mbinga,
Senyi Ngaga naye amethibitisha juu ya tukio hilo na kusema; “nimemwagiza
OCD wa Mbinga, ahakikishe uchunguzi wa kina unafanyika na watuhumiwa
waliohusika katika tukio wanakamatwa na taarifa zaidi tutaendelea kuzitoa baadaye
ni wangapi, waliohusika katika jambo hili”, alisema Ngaga.
Aidha alipohojiwa kwa niaba ya
wenzake, mwandishi wa habari Nyandindi alisema kuwa yeye alinusurika kupigwa
lakini aliokolewa na mtendaji wa kata hiyo ya Ruanda, Dominick Komba kwa kumhifadhi
ndani ya nyumba yake ambayo ipo kijijini humo.
“Wakati kundi hili linawasili katika
eneo la ofisi za kata ambako sisi waandishi wa habari tulikuwa tunafanya
mahojiano na viongozi wa kata hiyo, ghafla tulijikuta tumezingirwa na kikundi
hicho huku wengine wakipaza sauti wakisema sisi ni wafuasi wa Mbunge Kayombo
hatuhitaji waandishi wa habari hapa kijijini kwetu ondokeni haraka sana, huku
wengine wakileta fujo”, alisema Nyandindi.
Kwa upande wa waandishi wa habari wa
redio Jogoo, katika kunusuru uhai wao walikimbia na kwenda kujificha nyumba
jirani, zilizopo katika kijiji hicho.
Nyandindi aliongeza kuwa vurugu hizo
zinatokana na mvutano wa kisiasa uliotawala katika kata hiyo ambao
umesababishwa na Mbunge Kayombo, kutokana na kudondoka kwenye uchaguzi wa kura
za maoni kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), hivyo kikundi hicho
kimekuwa kikiendeleza vurugu kijijini hapo na kusababisha kufunga makufuli
katika ofisi za serikali za kata ya Ruanda.
“Baada ya kujinusuru na mkasa huu,
tulikwenda kuripoti kituo kikuu cha Polisi wilaya ya Mbinga, tumefungua jalada
la kesi lenye namba MBI/IR/1370/2015 ambapo tunaviachia kazi vyombo vya dola
viendelee kutekeleza majukumu yake ili sheria iweze kuchukua mkondo wake
ikiwemo watuhumiwa waliohusika na tukio hili wakamatwe na kufikishwa
Mahakamani”, alisema.
Hata hivyo jitihada za mtandao huu za
kumpata aliyekuwa mbunge wa jimbo la mbinga mashariki Gaudence kayombo
ziligonga mwamba baada ya kupigiwa simu ya kiganjani kuto pokelewa.
Chapisha Maoni