0


                 


       NA STEPHANO MANGO, SONGEA
MGOMBEA wa nafasi ya Udiwani kupitia tiketi ya Chama cha ACT Wazalendo kata ya Majengo iliyopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma Bakari Likapo,amesema kuwa endapo wananchi watampa ridhaa ya kuwatumikia atahakikisha posho zake zote zinazotokana na vikao vya Baraza la Madiwani zitatumika kwa ajili ya kuchangia mfuko wa maendeleo ya kata hiyo


Likapo aliyasema hayo jana mwishoni mwa wiki wakati alipokuwa akiwahutubia wananchi waliofika kumsikiliza kwenye mkutano wa uzinduzi wa kampeni ya kata hiyo uliofanyika katika viwanja vya Transfoma Majengo mjini Songea.



Alisema kuwa sababu kubwa iliyomsukuma kuchangia mfuko huo wa maendeleo utakaoundwa katika kipindi cha uwakilishi wake ni kwa ajili ya kusaidia makundi mbalimbali yasiyojiweza ikiwemo watoto Yatima,wajane,wazee wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za kununua pembejeo za kilimo,vijana pamoja na kuwalipia ada watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.



Aidha kati ya mambo mengine aliyoahidi kuwatekelezea wananchi wa kata hiyo kuwa ni kuanzishwa kwa viwanda vidogo vidogo ambavyo vitasaidia kutoa ajira kwa vijana,kutoa mikopo ya pikipiki kwa masherti nafuu kwa waendesha bodaboda,kupiga marufuku michango mbalimbali isiyokuwa ya lazima kwenye shule za msingi pamoja na kupambana na tatizo la kukithiri kwa takataka katika maghuba.



Naye Mwenyekiti wa  wa chama cha ACT Wazalendo mkoa wa Ruvuma,Mohamed Kudeka amewatahadharisha wananchi kuacha kugombanishwa na bendera za vyama vya siasa badala yake wametakiwa kuwachagua viongozi wenye fikra na mtazamo wa kimaendeleo na sio wacheza bao.



Hata hivyo mgombea Udiwani  kupitia tiketi ya chama hicho kata ya Misufini Manispaa ya Songea mkoani humo Delux Mayono amewataka wananchi kuacha kuwachagua viongozi wanaotokana na chama cha Mapinduzi(CCM)kwa madai kuwa chama hicho kimekuwa maarufu wa kuzalisha na kutengeneza mafisadi ambapo Ukawa ni wanunuzi wa mafisadi hao.



Kwa upande wake mmoja wa kada wa Chama cha Mapinduzi(CCM)wa kata ya Majengo Tumaini Msumba,ambaye alifika kusikiliza Sera za chama hicho kwenye mkutano huo wa ACT  alipopewa nafasi ya kusalimia,aliwataka wananchi kuacha ushabiki wa vyama vya siasa na badala yake wajitokeze kwa wingi  kugombea nafasi za uongozi na kusikiliza sera za vyama mbalimbali kwa ajili ya kuwapima wagombea watakaofaa kuwaongoza.



MWISHO

Chapisha Maoni

 
Top